
Waziri wa maji katika kaunti ya Isiolo, Ali Wario amesifia uzinduzi huo wa maji katika kijiji cha Jillo Dima, akisema kuwa maji hayo yatawasaidia wakaazi katika kijiji hicho kutumia maji safi kwa afya zao.
Ameongezea na kusema kuwa, kujengwa kwa bwawa la maji katika eneo la Kubikalo katika kaunti hiyo, kando na mto Ewaso Nyiro kutasaidia kupatikana kwa suluhu la ukosefu wa maji katika eneo hilo.
“Yale magonjwa ambayo huwa mnaugua mkienda hospitalini yanachangiwa sana na unywaji wa maji machafu. Tukipata maji sai sasa, afya zetu zitaimarika na magonjwa yanayotokana na matumizi ya maji machafu hayatashuhudiwa,” Ali Wario, waziri wa maji katika kaunti ya Isiolo alisema.
Askofu katika jimbo la Nyambene, Gerald Kithure amesema kuwa kuna haja ya wadi ya Kinana na maeneo mengine ya kaunti hiyo kujihusisha na kilimo cha unyunyizi maji mashamba. Ametoa wito kwa washikadau na maafisa kwenye serikali kusaidia maeneo hayo katika ukuzaji wa mimea ili kukabili ukosefu wa maji katika kaunti hiyo.
“Watu wetu watapata chakula cha kula, tukiendelea kuzindua visima vingi vya maji tutaimarisha zaidi ukuzaji wa mimea kutatua tatizo la uhaba wa chakula. Tutaweza kupanda mboga, parachichi ambazo huhitajika sana katika taifa la china na pia maembe ambayo yanafanya vizuri katika maeneo haya. Tuna imani tutakuwa na faida nyingi,” askofu wa Nyambene, Gerald Kithure alisema.
Mashirika hayo yamehimiza pia kusafishwa kwa maji ya visima ili wakazi wapate maji safi ya kutimia bila kushuhudiwa kwa madhara yoyote ya kiafya. Maeneo ya kaskazini na mashariki ya humu nchini yamekuwa yakishuhudia uhaba na ukosefu wa maji na chakula ,kutokana na janga la ukame. Hata hivyo, serikali na wahisani wametoa misaada mbalimbali ili kuwasaidia waathiriwa.
Na James Chacha