
Utekelezaji wa mtaala wa CBC upo kwenye mwaka wa sita huku wanafunzi wa gredi ya sita wakitarajia kujiunga na sekondari ya ngazi ya chini mwezi Januari mwaka ujao, licha ya safari hiyo, maswali yangalipo kuhusu ufaafu wa CBC, huku rais Ruto akitangaza kubuni mpango wa jopo kazi la kutathmini CBC.
Wadau kwenye sekta ya elimu wamekuwa wakiishtumu wizara ya elimu, kwa kuendesha CBC kwa siri pasi na kuwahusisha wote.
Hata hivyo kupitia jarida lake la kwanza kuhusu cbc na utekelezaji wake. Wizara ya elimu imetoa majibu ya moja kwa moja kwa madai hayo. Taarifa kwenye jarida hilo la kurasa 59, inakusudia kutoa na kuweka wazi taarifa au ufafanuzi kuhusu CBC, mbali na kuwawezesha wote wanaotaka kutoa hoja tofauti kujitokeza.
Aidha jarida hilo linaongeza kwamba lengo kuu, ni kuwezesha umma na wazazi kuelewa kung’amua, yanayoendelea. Jarida hilo limechapishwa na wizara ya elimu kwa kuzishirikisha sekta nyinginezo zinazohusika kwa utekelezaji wa cbc kama vile bodi ya kuajiri walimu (TSC), bodi ya usimamizi wa mitihani (KNEC) na bodi ya mtaala (KICD).
Na Joram Kitui